Friday, July 22, 2011

MAHOJIANO BAINA YA RAIS KIKWETE NA MWANDISHI WA BBC,OMARI MUTASA, YALIYOFANYIKA AFRIKA KUSINI WAKATI RAIS KIKWETE AKIENDELEA NA ZIARA YAKE YA KISERIKALI:

Rais wa jamhuri wa muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kiwete.

BBC: Suala la Umeme Mheshimiwa Rais Kikwete ungependa kulizungumzia nini?

Rais Kikwete: Tatizo la umeme kimsingi ni suala la ukame tu.Kwa sababu mabwawa yetu ya kuzalisha umeme yanayotoa umeme karibu MW600 sasa hivi yanatoa umeme kidogo sana. Maji pungufu ndio maana kuna tatizo hilo.

BBC:Mheshimiwa,hili suala si la leo wala si la jana limekuwepo kwa muda mrefu, kwanini serikali haina njia mbadala ya kuweza kutatua suala hili? Tanzania ina raslimali nyingi mheshimiwa Kikwete!

Rais Kikwete:Kwanza, serikali haina uwezo wa kufanya mvua inyeshe, unajua unajua hivyo, Kwa sababu (kicheko) ingekuwa na uwezo wa kufanya mvua inyeshe mabwawa yale yangejaa.Ni kweli kuwa Tanzania inazo raslimali za kutosha na katika kipindi hiki - toka wakati ule -sisi tulipoingia tumekuta suala la Ukame na mwaka 2007 tukapata matatizo ya kwanza.

Baada ya pale tukafanya uamuzi kwamba sasa tuanze kuwekeza katika vyanzo vingine; tuongeze uzalishaji wa umeme kutoka vyanzo vingine. Tuongeze uzalishaji wa umeme kutoka vya vya kutumia gesi asilia twende kwenye makaa ya mawe. Kutoka vyanzo vya gesi asilia tayari tuna mtambo pale Ubungo, na toka mwaka 2009 mpaka sasa tumeshaongeza MW145, itakapofika Disemba tutakuwa tumeongeza MW160 nyingine. Tutakuwa tumeongeza MW300 siyo kidogo.

BBC: Mhe. Kikwete Mmoja katika wabunge Bw. John Mnyika ambaye ni Mbunge wa upinzani ambaye ni Waziri Kivuli wa Nishati amekuwa akilalamika na kwamba amewahi kusema kwamba hili tatizo ni tatizo linalowahusu Watanzania wote na amesema mje pamoja na kuona vipi mtakavyotatua tatizo hili. Na sasa hivi Bungeni wamesimamisha mswada, wa kutoa bajeti ya nishati ya Tanzania. Wewe unachukulia vipi matamshi kama haya kutoka kwa Wabunge?

Rais Kikwete: Mimi nasema hivi yeye si Mbunge atoe maarifa yake tu; anayo maarifa gani na anapendekeza kitu gani. Kwa sababu toka Uhuru mabwawa tuliyotengeneza ni Kidatu MW200, Mtera MW80, Kihansi MW 165 mimi nilipokuwa Waziri wa Nishati, pale Pangani tumeongeza.
Sasa ufikirie kwamba toka Uhuru tumeweza kuzalisha umeme wa MW600, lakini toka 2009 mpaka Disemba mwaka huu tutakuwa tumeongeza MW300! Ni jitihada kubwa. Mimi nasema kwamba usipozitambua hizo ni kwamba wewe mwenyewe siyo mkweli.

Sasa ni hivi, unajua hii mitambo ya umeme si mitambo unaenda kununua kama unavyonunua jaketi lako hili. Ni kwamba ukitaka mitambo ya umeme, lazima uweke order wakutengenezee. Huu mtambo unaofika mwaka huu Disemba order tuliweka mwezi wa Juni mwaka jana. Inachukua muda huo kutengeneza. Sasa ingekuwa mnaenda kutafuta mitumba, mitumba ya mitambo tu ya kununua iko mingi kweli. Tukasema hatuwezi kufanya hivyo.

Mimi nasema hivi, kitu kikubwa ni kuwa na subira. Tumefanya jitihada kubwa. Ni lazima watu watambue kuwa tumefanya jitihada kubwa katika miaka hii toka 2009 mpaka sasa hivi 2011 Disemba tutakuwa tumeongeza MW300 kulinganisha na MW600 ambazo tumeziongeza katika miaka yote hii. Nasema ni lazima watu watambue hivi. Sasa kama kuna mtu ana maarifa ya haraka zaidi nasema mtu atoe maarifa hayo na sisi kama yapo tutayafanyia kazi.

BBC: Kuna njia kama umeme wa jua, umeme wa kutokea ardhini wa mvuke, kwanini serikali haitafuti njia mbadala kuzalisha umeme kwa njia hizo?

Rais Kikwete: Nasema hivi, hata umeme wa jua lazima ujenge, umeme wa mvuke lazima ujenge, si kitu cha mwezi mmoja. Nasema huo ndio ukweli wenyewe na wakati mwingine na nyinyi mjifunze hayo mambo ya kitaalamu kulikoni kuuliza tu hivi hivi. Unajua ungekuwa na wewe unauliza kwa hoja - “unajua kwamba hiki kitu hiki ingekuwa umeme wa jua miezi miwili tu upo” - tungeweza kufanya hivyo.

Sisi sasa hivi kwa mfano tunajiandaa kuzalisha umeme wa kutumia Upepo, pale Singida. Tuna mwaka wa tatu sasa tuna mipango na Wakorea wa Kusini,umeme haujakuwepo.Kwa hiyo nasema hayo ni maelezo rahisi. Wanasema “mbona jua lipo?” katengeneze umeme wa jua kama jua lipo!(kicheko).

BBC: Watanzania wamekuwa wakisema (mwisho kabisa) kwamba Tanesco ingebinafsishwa ili waweze kupata makampuni kufanya kazi hiyo ya umeme?

Rais Kikwete: Aah! Kwani ukitaifisha kesho ndio utapata mitambo kesho? Nasema hivi ni vizuri kuelewa tu - kwanza tatizo la msingi - ni maji kukauka kwenye mabwawa. Maji yasingekauka kwenye mabwawa tatizo hili halipo. Maji yamekauka kwenye mabwawa kwa sababu ya ukame. Hakuna mtu mwenye uwezo wa kuzuia ukame usiwepo. Sasa hiki ndicho kiini cha tatizo. Sasa nasema sisi jitihada ambayo tumeifanya ni kupunguza sasa kutegemea umeme unaotakana na nguvu ya maji.

Toka mwaka 2009 tumewekeza adi Disemba 2011 tutakuwa tumeongeza MW 310, yenyewe hiyo ni hitihada kubwa, ni vizuri ukaitambua jitihada hiyo. Kulikoni kusema kitu tu nasema hatakam huna majawabu rahisi utuambie tu.

MWISHO.

 Note: To post a comment:
Click 'comment',write your comment in the comment pad,THEN (Select Anonymous profile to hide your name OR Name/URL profile to disclose your name ie Name: (Write your name) and URL: (This is optional)) THEN Click 'Post comment',type the word shown for verification THEN Click 'Post comment'.

1 comment:

  1. Huyo jamaa kikwete hana jipya bana, urais umebaki jina tu kwake nchi imeshamshinda, hana jipya.

    ReplyDelete