Wednesday, November 16, 2011

BAADA YA KUTOKA KWA DHAMANA, MBUNGE WA ARUSHA MJINI (CHADEMA), GODBLESS LEMA, APOKEWA KWA KISHINDO HAPO JANA:

Mbunge wa jimbo la Arusha mjini,Godbless Lema,akiwa juu ya gari lake nje ya uwanja wa Mahakama Kuu kanda ya Arusha,baada ya kupata dhamana katika kesi ya kufanya maandamano na kufanya mkusanyiko bila kibali cha polisi. Picha na Filbert Rweyemamu
--
SHUGHULI mbalimbali za kibiashara na kijamii katika Jiji la Arusha jana zilisimama kwa muda kupisha mapokezi ya Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema baada ya kutoka rumande katika Gereza la Kisongo alilokaa kwa siku 14.Oktoba 31, mwaka huu, Lema na wenzake 18 walifikishwa mahakamani wakidaiwa kufanya kusanyiko lisilo halali na kukaidi amri ya polisi iliyowataka watawanyike yeye na wenzake.Walikamatwa na kufikishwa mahakamani na kudhaminiwa lakini Lema akikataa dhamana akisema ameamua kutangulia gerezani kudhihirisha kwamba haogopi gereza.Lema alitoka kwa dhamana na kuandaliwa mapokezi makubwa ya wafuasi wa Chadema ambayo yaligeuka kuwa maandamano ya amani.Shamrashamra za mapokezi hayo zilisababisha kusimama kwa muda kwa shughuli kadhaa kama huduma za kibenki hasa zile zilizo katika Barabara ya Sokoine.

Wakati wa maandamano hayo wafuasi hao wa Chadema walikuwa wakipeperusha majani na matawi ya miti.
Mahakimu, mawakili na makarani wa mahakama nao walilazimika kuacha shughuli zao kwa muda na kutoka nje kushuhudia mapokezi ya mbunge huyo yaliyokuwa yakipambwa kwa nyimbo mbalimbali nje ya mahakama hiyo.

Sehemu ya nyimbo hizo zilimgusa Mkuu wa Polisi Wilaya hiyo ya Arusha, Zuberi Mwombeji ambaye hivi karibuni aliingia kwenye mvutano mkubwa na chama hicho cha upinzani akituhumiwa kutumia nguvu kuwadhibiti viongozi wake.Waliimba: “Tunamtaka….panya wetu… tunamtaka mbunge wetu… Zuberi (OCD), aondoke. Mlituvizia usiku, leo sasa ni mchana hapatatosha. Hatuandamani, tunampokea shujaa wetu.”
 
Shamrashamra hizo pia ziliambatana na mabango mbalimbali huku pia kukiwa na fulana maalumu zilizokuwa zimevaliwa na baadhi ya mashabiki zikiwa na maneno yaliyosomeka: “Lema kaonyesha njia mbadala ya kudai haki. Jela ni mahali pa kuishi kama sababu ya kwenda huko ni vitadhidi uonevu, ukandamizaji wa haki na utu wa binadamu.” 

No comments:

Post a Comment